Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, June 28, 2013

Obama aendelea na safari yake Afrika

Rais Barack Obama wa Marekani atawasili leo nchini Afrika Kusini katika awamu ya pili ya safari yake barani Afrika. Akiwa nchini humo Obama atakutana na kufanya mazungumzo na mwenyeji wake Rais Jacob Zuma na kushiriki kwenye mkutano wa waandishi wa habari.
Safari ya Rais wa Marekani barani Afrika ambayo itagharimu yapata dola milioni mia moja, imegubikwa na hali mbaya ya kiafya ya rais wa zamani wa Afrika Kusini Mzee Nelson Mandela. Akiwa katika awamu ya kwanza ya safari yake barani Afrika, Obama alisema mjini Dakar, Senegal kuwa Mandela ni shujaa wa dunia ambaye iwapo atafariki dunia urithi wake utabakia kwa kipindi cha muda mrefu.

Duru za ndani ya ikulu ya Marekani White House zinasema kuwa mipango ya kukutana Barack Obama kama Rais wa kwanza mweusi wa Marekani na Nelson Mandela kama rais wa kwanza mweusi katika historia ya kisiasa ya Afrika Kusini imekuwa ikiahirishwa mara kwa mara na watu wa familia wa shujaa huyo wa Afrika. Obama aliwahi kukutana na Mzee Mandela mwaka 2005 alipokuwa Seneta katika Baraza la Seneti la Marekani pindi Mandela alipokuwa safarini mjini Washington.
Tangu mwaka 2008 wakati Barack Obama alipoteuliwa kuwa mgombea urais wa Marekani kwa tiketi ya chama cha Demokrats, watu wa Afrika walikuwa na matumaini makubwa na mwanasiasa huyo. Waafrika walitaraji kuwa, bara lao hususan nchi za chini ya jangwa la Sahara, lingepewa kipaumbele katika siasa za nje za Obama. Hata hivyo kiongozi huyo alikwenda kinyume kabisa na matarajio ya Waafrika katika awamu ya kwanza ya uongozi wake kati ya mwaka 2008 hadi 2012 na alilitembelea bara hilo mara moja tu kwa kufanya safari nchini Ghana. Wakati huo walimwengu hususan watu wa Kenya, walitaraji kwamba Obama ambaye ana asili ya Kenya, angetembelea nchi hiyo, jambo ambalo halijafanyika hadi hii leo.
Weledi wa masuala ya siasa wanasema kuwa, safari ya sasa ya Rais Obama wa Marekani barani Afrika ni fursa mwafaka ya kujaribu kuimarisha satua ya Washington barani humo katika mipango ya muda mrefu ya Marekani. Hususan ikitiliwa maanani kwamba, China na Brazil zinaongoza kwa kuwa na satua kubwa zaidi ya kiuchumi na kisiasa barani Afrika na sasa ni wakati wa Washington kufidia nakisi hiyo.
Kasi ya ustawi wa kiuchumi wa baadhi ya nchi za Kiafrika katika miaka ya hivi karibuni imeifanya Marekani ilikodolee macho zaidi bara hilo. Katika mtazamo huo Afrika Kusini ambayo ndiyo nguvu kubwa zaidi ya kiuchumi na kisiasa barani Afrika, inapewa nafasi maalumu katika saisa za nje za Marekani.

No comments: