Mkuu wa jeshi la Uganda, Jenerali
Katumba Wamala amewataka raia wa nchi hiyo kuchukulia kwa uzito indhari
zinazotolewa na polisi mara kwa mara kuhusu uwezekano wa kutokea
mashambulizi ya kigaidi. Jenerali Wamala amekumbusha kwamba, wanamgambo
wa al-Shabab bado wanaiangalia Uganda kwa jicho la hasira kutokana na
nchi hiyo kuwa na wanajeshi nchini Somalia. Amesema polisi wanapotoa
tahadhari huwa wamefanya uchunguzi na kupata taarifa za kuaminika za
kiintelijensia na kwa mantiki hiyo haifai wananchi kupuuza tahadhari
hizo.
Polisi ya Uganda imetangaza kuongeza
maafisa wa usalama wanaopiga doria mjini Kampala ili kuepusha uwezekano
wa nchi kushambuliwa na magaidi. Polisi ya nchi hiyo pia imetangaza
ratiba maalum ya doria wakati wa mashindano ya kombe la dunia katika
mchezo wa soka yanayotarajiwa kuanza baadaye mwezi ujao nchini Brazil.
Itakumbukwa kuwa, mwaka 2010 wanamgambo wa al-Shabab walishambulia kwa
mabomu kumbi kadhaa za starehe mjini Kampala wakati wa mechi ya fainali
ya kombe la dunia ambapo zaidi ya watu 70 waliuawa.







No comments:
Post a Comment