Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, May 21, 2014

Zaidi ya watu 100 wauawa kwenye milipuko Nigeria

Takriban watu 118 wameuawa kwenye milipuko miwili ya mabomu katika mji wa Jos ulioko katikati mwa Nigeria. Habari zinasema milipuko hiyo imetokea kwenye kituo kimoja cha mabasi mjini hapo jana Jumanne. Mratibu wa Ofisi ya Kitaifa ya Misaada ya Dharura, Mohammed Abdulsalam amesema idadi ya vifo inaweza kuongezeka kwani inaaminika kuna watu wengi waliofunikwa chini ya vifusi baada ya magari kuanguka na baadhi ya majengo kuporomoka kutokana na kishindo cha milipuko hiyo.
Hadi sasa hakuna mtu au kundi lililodai kuhusika na shambulizi hilo lakini baadhi ya watu wanalinyooshea kidole cha lawama kundi la Boko Haram ambalo katika siku za huko nyuma limewahi kukiri kutekeleza mashambulizi ya aina hiyo.
Rais Goodluck Jonathan ametoa taarifa ya kulaani mashambulizi ya hapo jana na kuyataja kuwa ya kinyama na ya kishetani. Amesema serikali haitapigishwa magoti na magaidi na kwamba kila juhudi zitafanywa ili kuwakamata wahusika. 

No comments: