Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Thursday, June 12, 2014

Nchi za Afrika Mashariki zasoma bajeti ya 2014/2015

Mawaziri wa Fedha wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamesoma bajeti za nchi zao mbele ya wabunge leo alasiri. Bajeti hizo zinazoainisha jinsi serikali za nchi hiyo zitakavyotumia fedha za umma katika mwaka 2014/2015 zimetoa vipaumbele tofauti kutoka nchi moja hadi nyingine.
Nchini Kenya, Waziri wa Fedha, Henry Rotich amesoma bajeti ya Shillingi Trilioni 1.8 ambapo sekta za Elimu na Usalama wa Taifa ndizo zilizopata kiwango kikubwa cha fedha.
Akisoma bajeti hiyo mbele ya wabunge, Waziri Rotich amesema wizara yake imeamua kutoa kipaumbe cha kwanza kwa elimu kutokana na ahadi ya serikali ya kuboresha sekta hiyo kwa lengo la kuinua kiwango cha elimu nchini. Waziri huyo amesema bajeti inatazamiwa kukua hadi asilimia 6.8 mwaka ujao wa 2015.
Huko Uganda, Waziri wa Fedha, Maria Kiwanuka amesoma bajeti ya Shilingi trilioni 14 ambapo sekta za kazi na uchukuzi ndizo zilizopata kitita kikubwa cha fedha. Waziri Kiwanuka amesema serikali ya Kampala ina nia ya kurahisisha usafiri wa bidhaa na watu ndani na nje ya Uganda na kwa mantiki hiyo imeonekna pana haja ya Wizara ya Uchukuzi kutengewa fedha zaidi. Bajeti ya mwaka uliopita ya Uganda ilikuwa ya trilioni 13.1
Bajeti ya Rwanda imetajwa kuwa ya Franga trilioni 1.75 ambapo Waziri wa Fedha, amesema nchi hiyo inakabiliwa na nakisi ya bajeti ya Franga bilioni 177.2. Kiwango kikubwa cha nakisi hiyo kitajazwa kutokana na mikopo ya ndani na nje ya nchi.
Mjini Dodoma, Tanzania, Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, amesoma Bajeti ya zaidi ya shilingi trilioni 19 ikiwa ni takriban asilimia 7 zaidi ikilinganishwa na ile ya mwaka uliopita ya trilioni 18.2. Waziri Saada Mkuya amesema serikali itafunga mianya inayotumiwa na wakwepaji kodi ili kukusanya kodi ya kutosha pamoja na kuweka mikakati itakayoleta nidhamu katika matumizi ya fedha za umma. Hii ni katika hali ambayo, Tanzania imekumbwa na kashfa kadhaa za ufisadi na utumiwaji mbaya wa fedha za umma katika kipindi cha miezizi sita iliyopita.

No comments: