Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Sunday, June 9, 2013

Wakwepa kodi wajitapa, hatua za TRA ni upepo

Hii ni baada ya serikali kutangaza kusitisha utoaji mizigo bila kukaguliwa katika bandari ya Dar es Salaam, wakwepa kodi wakubwa wamekejeli na kusema “ni nguvu ya soda na ni upepo tu utapita” kwa maelezo kwamba mtandao haujatetereka.
Habari kutoka kwa watu walio karibu na wafanyabiashara wanaotuhumiwa kukwepa kodi, zinaeleza kwamba wameanza kuikejeli hatua ya serikali na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kudhibiti mizigo inayoingia nchini kwa kudai kwamba hatua hiyo ni kupunguza kelele za watu waliowaita ‘wambea’.
“Wametuambia tusubiri muda si mrefu kazi ya kupitisha mizigo itaendelea maana mtandao wao uko pale pale na wataanza tena kutupitishia mizigo yetu kwa mtindo ule ule wa ‘direct release’.


“Tumewashitukia na sasa bora tupitie mkondo halali wa TRA badala ya kutuingizia hasara,” alisema mfanyabiashara wa Kariakoo, ambaye amejikuta akipata hasara baada ya mizigo yake kutozwa faini kubwa kwa kudanganya aina ya mizigo baada ya kupitia kwa wafanyabiashara waliobanwa sasa na TRA.
Baada ya gazeti hili kuandika mfululizo taarifa kuhusiana na ukwepaji kodi unaotumia utaratibu wa ‘ditect release’, TRA ilisitisha ghafla utaratibu huo na kuanza kufanya ukaguzi maalumu uliobaini ukwepaji mkubwa wa kodi unaofanywa na wafanyabiashara wachache wanaodanganya aina ya mizigo na hata thamani halisi.
Suala hilo likaibukia bungeni, siku chache baada ya Tanzania Daima kuandika Waziri wa Fedha, Dk. William Mgimwa, alivyoshitukia ukwepaji kodi huo.
Akihitimisha bajeti yake, Waziri Mgimwa, alisema serikali imesimamisha utaratibu wa utoaji wa mizigo moja kwa moja bandarini na kuanzia sasa mizigo yote itakaguliwa bila kujali nyaraka zitakazoonyeshwa.
Alisema hatua hiyo imekuja baada ya kugundulika kwa ukwepaji wa kodi kwa kutoa nyaraka tofauti na uhalisi wa mizigo iliyopo katika kontena husika kunakofanywa na baadhi ya makampuni ya kutoa mizigo katika bandari hiyo.
Alisema kutokana na udanganyifu huo, kuanzia sasa ukaguzi utafanyika kwa kuangalia aina ya mizigo, nchi iliyotoka, muhusika wa mzigo, na historia ya mtoaji wa mzigo bandarini.
Kama ilivyoandikwa na Tanzania Daima katika habari yake ya uchunguzi, Waziri Mgimwa alisema kutokana na kugundulika kwa udanganyifu huo kati ya makontena 522 yaliyokuwepo 498 yalikaguliwa upya.
Waziri huyo alisema kati ya makontena hayo yaliyokaguliwa upya, ilibainika kuwa 188 yalikuwa na nyaraka zinazoonyesha mizigo tofauti na iliyokuwemo ndani ya makontena hayo na kwamba serikali ilipata sh bilioni 1.24.
Katika taarifa ya Waziri Mgimwa inayothibitisha taarifa zilizochapishwa na gazeti hili, makontena yaliyobainika kufanya udanganyifu, yalikutwa na mizigo ya ziada aina tofauti na mizigo iliyojazwa katika karatasi, wajazaji wengine kudai wana mzigo mdogo thamani halisi ya mzigo.
Ilibainika kwamba bidha zilizobainika katika makontena hayo ni pamoja na CPU, vyandarua (kwa sababu havitozwi ushuru), monitor za kompyuta, solar panel (vifaa vya uzalishaji wa umeme wa jua), aluminiam na nguo.
Alisema serikali imegundua kuwa kuna udanganyifu unatumia mtandao wa nyaraka feki katika kuondoa mizigo bandarini kwa kushirikiana na mawakala wa usafirishaji na uondoshaji mizigo bandarini ambao si waaminifu.
Katika maelezo yake bungeni, Mgimwa alisema serikali imeweza kuinasa baadhi ya mihuri ya mawakala wanaoshughulika na utoaji wa mizigo bandarini ambayo ni bandia.
Mbali ya udanganyifu huo, Tanzania Daima imebaini pia kuwapo kwa mbinu chafu za kuiibia serikali mapato kwa njia ya mtandao zilizokuwa zikifanywa na baadhi ya wafanyabiashara wanaopitishia mizigo yao bandari ya Dar es Salaam, kabla ya TRA kugundua na kufanya mabadiliko makubwa katika mfumo wake wa mtandao unaotumika kuidhinishia mizigo.
Taarifa hizo zilizothibitishwa na maofisa waandamizi wa TRA, zilieleza kwamba wafanyabiashara hao ambao wanatajwa sana katika sakata la ukwepaji kodi, walifanikiwa kuingia katika mtandao wa TRA na kuwa wanabadili alama maalumu zinazoonyesha mizigo inaruhusiwa kupita bila kukaguliwa.
Tayari kumekua na taarifa za mmoja wa wafanyabiashara anayetajwa kuhusika na ukwepaji kodi ameamua kukimbilia nje ya nchi kukwepa hatua zinazoweza kuchukuliwa dhidi yake.
Mbali ya mfanyabiashara huyo kutajwa kukimbia, taarifa zinaeleza kwamba kuna wafanyabiashara kadhaa wa maeneo mbalimbali nchini ambao wamepata mshituko mkubwa baada ya kubaini kwamba walikuwa wanawatumia wafanyabiashara hao kukwepa kodi huku wengine wakifilisika baada ya TRA kufanya ukaguzi upya wa mizigo yao.
Kampuni inayotajwa kuhusika kwa kiasi kikubwa inatajwa kuwa ni ile maarufu kwa uuzaji wa bidhaa za nyumbani na wahusika wanaelezwa kujisahau sana na kufanya hadharani kwa kutumia majina ya vigogo wa juu serikalini.
Kwa takriban miaka mitatu iliyopita serikali kama njia ya kuondoa mizigo bandarini mapema kwa kuepusha mrundikano na msongamano wa mizigo bandarini, iliruhusu baadhi ya mizigo ya wateja wakubwa iwe inachukuliwa bila kukaguliwa.
Kitendo hiki japo kilionekana kuwa na lengo nzuri, kilikosolewa na wengi kwa kile kilichoonekana kingeweza kikatumiwa vibaya na baadhi ya wateja wakubwa kwa kukwepa kulipa kodi stahiki.

No comments: