Serikali ya Nigeria imekataa pendekezo
lililotolewa na kundi la kigaidi la Boko Haram la nchi hiyo lililoitaka
serikali ibadilishane nalo wanamgambo wa kundi hilo wanaoshikiliwa
kwenye jela za serikali, na mabinti liliowateka nyara hivi karibuni.
Huku akionyesha mkanda wa video wa mabinti kadhaa waliokuwa wakisoma
Qur'ani, Abubakar Shekau kamanda wa wanamgambo wa Boko Haram amedai kuwa
mabinti hao ni wale waliotekwa nyara na wanamgambo hao tarehe 14 Aprili
huko katika mji wa Chibok ulioko katika jimbo la kaskazini mwa Nigeria
la Borno. Ujumbe wa mkanda huo unasema kuwa mabinti hao ambao wote
walikuwa Wakristo sasa wamesilimishwa na wanamgambo wa Boko Haram.
Abubakar Shekau ameiambia serikali kwamba yuko tayari kuwaachilia huru
mabinti hao wote 223 iwapo serikali itawaachilia huru wanamgambo wa Boko
Haram wanaoshikiliwa katika jela za serikali. Mabinti 276 walikuwa
katika shule ya bweni ya Chibok ilipovamiwa na Boko Haram lakini baadhi
yao walifanikiwa kukimbia na kuokoa maisha yao wakati wa kutekelezwa
uvamizi huo. Baadhi ya wachambuzi wa mambo wanasema kuwa huenda
pendekezo hilo la Boko Haram likakubaliwa na serikali baadaye iwapo
litaonekana kuwa na maslahi kwa jamaa za mateka na serikali ya Abuja.
Shehu Sani mtaalamu kuhusiana na kundi
la Boko Haram anasema kuwa washukiwa wanaofungamana na kundi la Boko
Haram wanagawanyika katika makundi matatu ya makamanda wa ngazi za juu,
askari wanamgambo na watu wa karibu pamoja na familia za makamanda wa
Boko Haram. Sani anaamini kwamba huenda serikali ya Nigeria ikaliachilia
huru kundi hili la tatu yaani wanawake na mabinti wa watu
wanaofungamana na Boko Haram ili kuonyesha nia yake njema kwa kundi
hilo. Pendekezo kama hilo la kuachiliwa huru wafungwa wa kisiasa wa Boko
Haram pia lilitolewa mwaka uliopita. Wakati huo, ni familia za watu
wanaozungumza Kifaransa wa Kaskazini mwa Cameroon ndio waliokuwa
wametekwa nyara na Boko Haram na ziliachiliwa huru baada ya kufanyika
mazungumzo kati ya wawakilishi wa kundi hilo na gavana wa jimbo la Kano
la Nigeria. Wakati huohuo, wataalamu wengine wa mambo wanasema kuwa
pendekezo hilo la Abubakar Shakeu la kubadilishana mateka na wafungwa wa
Boko Haram ni alama ya kulegeza msimamo wake wa hapo awali.
Tukio la kutekwa nyara wasichana
waliotajwa wa shule na kundi la kigaidi la Boko Haram, tukio la kinyama
ambalo limelaaniwa vikali na taasisi pamoja na serikali nyingi za dunia,
ni jambo ambalo lilikuwa halijawahi kutekelezwa na kundi hilo tokea
lianzishe mapambano ya silaha dhidi ya serikali ya Abuja mwaka 2009. Kwa
kuzingatia uungaji mkono wa kimataifa kwa serikali ya Nigeria dhidi ya
Boko Haram, huu ni wakati muafaka kwa serikali kupambana vilivyo na
kundi hilo na kuwathibitishia walimwengu upotofu wa fikra zake, kundi
ambalo linalochafua jina la Uislamu kwa kujihusisha na vitendo vya
kigaidi dhidi ya watu wasio na hatia. Wataalamu wa mambo wanaamini kuwa
kama serikali ya Nigeria haitachukua hatua za dharura na za haraka kwa
lengo la kuwakomboa mabinti hao mateka bila shaka jambo hilo litaandaa
uwanja mzuri kwa ajili ya nchi za Magharibi kama vile Ufaransa,
Uingereza na Marekani kuingilia mambo ya ndani ya nchi hiyo. Kwa sasa
nchi hizo zinautazama utajiri mkubwa wa maliasili wa Nigeria kwa jicho
la tamaa na kwa hivyo ziko tayari kutumia kisingizio chochote kile
kupora utajiri huo kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja.







No comments:
Post a Comment