Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, May 21, 2014

Kuakisiwa mizozano na mivutano ya wapinzani wa Syria

Mizozo na mivutano kati ya makundi ya upinzani yanayobeba silaha nchini Syria inazidi kuongezeka siku baada ya siku. Kushtadi migogoro hiyo kunakwenda sambamba na mafanikio makubwa ya jeshi la Syria katika kupambana na magaidi nchini humo.  Kuhusiana na hilo, As'ad Mustafa Waziri wa Ulinzi wa serikali eti ya muda ya wapinzani amelazimika kujiuzulu baada ya kuzuka hitilafu kubwa kati yake na Ahmad Jurba mkuu wa muungano unaojiita Syrian National Coalition (SNC).
Kabla ya hapo Sami Al-Oraidi kiongozi wa kundi la Jabhat an-Nusra alisema kuwa, Ahmad Jurba mkuu wa Muungano wa Kitaifa wa Syria SNC ameiba dola milioni 75 zilizotolewa kama msaada kwa makundi ya upinzani nchini Syria.
Vile vile sambamba na kushadidi hitilafu na mivutano baina ya makundi ya kigaidi yaliyoko Syria, Riyadh As'ad mwasisi wa kundi la kigaidi la Jeshi la Ukombozi wa Syria naye ametoa wito wa kuvunjwa kundi hilo akisema kwamba, viongozi wake hawana wanachofikiria ghairi ya pesa na madaraka. Wachambuzi wa mambo wanaamini kwamba, licha ya kuweko misaada ya madola ya Magharibi na Saudi Arabia kwa magaidi wa Syria, lakini mwenendo wa kushindwa magaidi na jeshi la Syria unaendelea kushuhudiwa na kuonekana zaidi kadiri siku zinavyosonga mbele, jambo ambalo linatajwa na wajuzi wa mambo kwamba, limewafanya viongozi wa makundi hayo ya kigaidi wachanganyikiwe na kuanza kuparurana wao kwa wao. Aidha katika mlolongo wa kushadidi hitilafu kati ya wapinzani wa Syria, hivi karibuni  kundi la kigaidi linalojiita Serikali ya Kiislamu ya Iraq na Sham (DAESH) lilimuua kwa kumkata kichwa mmoja wa viongozi wa kundi jingine lilalojulikana kwa jina la Ukombozi wa Sham. Hii ni katika hali ambayo, chombo kimoja cha habari cha Uingereza kimefichua jinai za kutisha zinazofanywa na makundi ya kigaidi ya Syria na kubainisha kwamba, vitendo vya makundi hayo vinashahibiana na makundi ya kimafia. Duru za Syria kwa upande wake zimeashiria juu ya kutokuweko malengo mamoja kati ya makundi ya kigaidi nchini humo na kufichua pia mizozo iliyopo hivi sasa kati ya nchi zinazoyaunga mkono makundi hayo ya kigaidi na kusisitiza kwamba, kile ambacho leo kinatokea nchini Syria ni ugaidi wa kimataifa wa baadhi ya nchi za Kimagharibi na Kiarabu.
Ukweli wa mambo ni kuwa, kadiri siku zinavyosonga mbele, ndivyo yanavyothibitisha wazi maneno ya viongozi wa Syria kwamba, nchi hiyo iko katika vita na makundi ya kigaidi ambayo yanapata himaya na uungaji mkono kutoka kwa madola ya Magharibi yanayodai kuwa vinara wa kutetea haki za binadamu ulimwenguni.

No comments: