Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Wednesday, May 21, 2014

Jeshi lashika hatamu na kuweka sheria kali Thailand

Jeshi la Thailand jana Jumanne lilitangaza kushika majukumu ya kulinda nchi lakini limesisitiza kuwa hatua hiyo si mapinduzi ya kijeshi. Habari zinasema jeshi limetangaza sheria kali ikiwa ni pamoja na kutishia kuwatia mbaroni wanaochochea fujo pamoja na kuzuia vyombo vya habari kutangaza baadhi ya mambo. Mkuu wa jeshi la Thailand, Prayuth Chan-Ocha amesema kwa sasa masuala yote ya usalama yako mikononi mwa jeshi na amezitaka pande za kisiasa zinazohasimiana kufanya mazungumzo mara moja na kutatua hali ya mambo.
Pia kanali 10 za televisheni zimefungwa kwa muda. Waziri Mkuu wa serikali ya mpito ya nchi hiyo, amesema jeshi halikumshauri kabla ya kuchukua udhibiti wa nchi.
Maandamano makubwa yameshuhudiwa nchini Thailand kwa miezi 6 iliyopita ambapo wafuasi wa upinzani na wale wa serikali wamekuwa wakikabiliana katika mji mkuu, Bangkok. Maandamano hayo yaliyogubikwa na ghasia yamesababisha zaidi ya watu 25 kupoteza maisha. Wapinzani wamekuwa wakishinikiza Waziri Mkuu, Yingluck Shinawatra, ajiuzulu huku wafuasi wa mwanasiasa huyo wakisisitiza kuendelea utawala wake. Hata hivyo, mwanzoni mwa mwezi huu, mahakama ya kilele ilimuuzulu Bi. Shinawatra baada ya kumpata na hatia ya kutumia vibaya mamlaka yake.

No comments: