Waziri wa Waqfu na Masuala ya Kidini wa serikali halali
iliyochaguliwa na wananchi huko Palestina ametahadharisha juu ya njama
mpya za utawala wa Kizayuni wa Israel za kutaka kuugawa msikiti wa
al-Aqsa. Ismail Ridhwan amelaani hatua ya walowezi wa Kizayuni ya
kuuvamia msikiti huo ambao ni kibla cha kwanza cha Waislamu na kusema
kuwa, Wazayuni wanalenga kuvuruga hali ya mambo katika mji wa Quds ili
wadhibiti kikamilifu Masjidul Aqsa. Hapo jana Jumanne, Walowezi wa
Kizayuni wakisaidiwa na jeshi la utawala ghasibu wa Israel walivamia
msikiti wa al-Aqsa kwa upande wa magharibi kupitia 'Babul Maghariba' na
kuvunjia heshima matukufu ya Waislamu kwenye msikiti huo. Msikiti huo
mtakatifu wa Waislamu umekuwa chini ya hujuma ya mara kwa mara ya
Wazayuni jambo linaloendelea kuwakera Waislamu kote duniani.
Huku Wapalestina wakikaribia kukumbuka miaka 66 tangu
utawala wa Kizayuni uzikalie kwa mabavu ardhi zao, utawala huo bandia
pamoja na walowezi wa Kizayuni wameweka mikakati ya kuwazuia kufika
katika msikiti wa al-Aqsa kwa ajili ya maadhimisho hayo.
Pia katika kukaribia safari ya Kiongozi wa Kanisa Katoliki
Duniani, Papa Francis huko Quds Tukufu inayokaliwa kwa mabavu, Utawala
wa Kizayuni umezuia kuwekwa mabango ya kumkaribisha kiongozi huyo wa
kidini huko. Hatua hiyo imeikasirisha mno jamii ya Wakristo huko Quds.
Dimitry Dalyani, Katibu Mkuu wa makundi ya Kikristo katika ardhi za
Wapalestina zinazokaliwa kwa mabavu amesema Waislamu na Wakristo wa
mjini Quds wanapaswa kushirikiana bega kwa bega kupinga njama za
Wazayuni za kutaka kuuyahudisha msikiti wa al-Aqsa na mji wa Quds kwa
ujumla.
Papa Francis I anatarajiwa pia kutembelea eneo la Beit
al-Laham au kwa jina jingine Bethlehem lililoko ukingo wa Magharibi wa
Mto Jordan na tayari maandalizi yamekamilika ili kumpokea kiongozi huyo
wa Kanisa Katoliki Duniani. Duru zinaarifu kuwa, Rais wa Mamlaka ya
Ndani ya Palestina, Mahmoud Abbas atakutana na Papa wakati wa ziara yake
hiyo ambapo watajadili njama zinazofanywa na Israel za kuharibu turathi
za kidini na kubadilisha muundo wa mji wa Quds. Hii ni katika hali
ambayo, Bunge la utawala haramu wa Israel limeandaa muswada wa sheria
unaolenga kuugawa msikiti wa al-Aqsa. Tayari muswada huo umekabidhiwa
baraza la mawaziri la utawala wa Kizayuni kwa ajili ya kuidhinishwa.
Sheria hiyo ikipitishwa, itatoa idhini kwa Mayahudi kuingia katika
msikiti huo na kuendeshea humo shughuli zao.
Utawala ghasibu wa Israel baada ya kughusubu mji wa Quds
kwenye vita vya siku 6 vya mwaka 1967 ulianza kuharibu matukufu ya
kidini ya Waislamu na Wakristo wa Palestina katika mji huo ikiwa ni
pamoja na Masjid al-Aqsa na kanisa mashuhuri zaidi mjini hapo.







No comments:
Post a Comment