
Mkuu wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA), Sepp Blatter, amesema kuwa
Qatar haikufaa kupewa fursa ya kuandaa mashindano ya kombe la dunia
katika mchezo wa soka mwaka 2022 kutokana na joto kali nchini humo
katika msimu wa joto. Blatter amesema FIFA ilishauriwa kuhusiana na hali
hiyo lakini kamati husika ikapitisha kwa wingi wa kura kwamba Qatar
iandae mashindano hayo. Amesema hilo lilikuwa kosa kubwa ingawa
amekumbusha kwamba kila mwanadamu hukosea wakati mmoja au mwingine. Hata
hivyo mkuu huyo wa FIFA amekanusha madai kwamba Qatar iliwahonga
maafisa wa kamati husika ili kupata nafasi hiyo. Sepp Blatter amesema
tuhuma hizo zina malengo ya kisiasa. Mashindano ya kombe la dunia katika
mchezo wa soka mwaka huu yatafanyika nchini Brazil, mwaka 2018
yanatarajiwa kufanyika nchini Russia na kisha 2022 yamepangiwa kufanyika
nchini Qatar ambapo itakuwa mara ya kwanza kwa nchi ya Mashariki ya
Kati kuyaandaa.






No comments:
Post a Comment