Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, July 1, 2013

Jumatatu, Julai Mosi, 2013

Leo ni Jumatatu tarehe 22 Shaabani mwaka 1434 Hijiria, inayosadifiana na Julai Mosi mwaka 2013 Miladia.
Siku kama ya leo miaka 51 iliyopita, nchi ndogo ya Burundi ilijitangazia uhuru wake. Ardhi ya Burundi pamoja na Rwanda ilikuwa sehemu ya makoloni ya Mjerumani huko Afrika Mashariki kuanzia mwaka 1899 hadi 1917. Baada ya Vita Vikuu vya Kwanza vya Dunia na kushindwa Ujerumani katika vita hivyo, Umoja wa Mataifa uliikabidhi Ubelgiji ardhi ya Burundi na mwaka 1946, ukatambuliwa rasmi utawala wa Ubelgiji kwa nchi hiyo. Mwaka 1962 Burundi ilipata uhuru ikiwa na mfumo wa utawala wa Kifalme. Hata hivyo miaka minne baadaye wapigania jamhuri walimuondoa madarakani mfalme na kuanzisha mfumo wa serikali ya jamhuri.

Siku kama ya leo miaka 53 iliyopita, sehemu mbili za Somalia ya Uingereza na ya Italia ziliungana na kuunda nchi moja ya Somalia yenye kujitawala. Karne kadhaa nyuma, Somalia iliwahi kujitawala kwa kipindi kifupi. Mwaka 1884 Uingereza iliiweka katika himaya yake sehemu ya ardhi ya nchi hiyo. Miaka mitano baadaye Italia nayo ikakoloni baadhi ya sehemu za Somalia. Harakati za mapambano za Muhammad Abdullah Hassan dhidi ya Waingereza kuanzia mwaka 1901 hadi 1920 hazikusaidia kitu. Mwaka 1950 Umoja wa Mataifa uliitaka Italia iandae mazingira ya kujitawala na kuwa huru Somalia.
Na miaka 51 iliyopita siku kama ya leo, nchi nyingine ya Kiafrika ya Rwanda ilipata uhuru. Rwanda ina historia inayofanana na jirani yake wa kusini yaani Burundi ambapo kabla ya nchi hizo kujitangazia uhuru zilikuwa zikikoloniwa na Ubelgiji. Mwaka 1973, Meja-Generali Juvenal Habyarimana aliingia madarakani baada ya kufanya mapinduzi yasiyo ya umwagaji damu. Baada ya mapambano mtawalia ya wapigania uhuru wa Rwanda, hatimaye mnamo mwaka 1962, nchi hiyo ilipata uhuru na kabila kubwa kabisa nchini humo la Wahutu likashika hatamu za uongozi wa nchi. Hata hivyo mwaka 1994 kulitokea mauaji ya kimbari ambapo zaidi ya watu laki 8 waliuawa wengi wao wakiwa ni wa kabila la Kitutsi.

No comments: