Wanadiplomasia wa ngazi za juu wa Iran na Marekani wanatazamiwa
kukutana wiki ijayo kabla ya duru mpya ya mazungumzo ya nyuklia kati ya
Jamhuri ya Kiislamu na madola sita makubwa duniani.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imetoa taarifa na kusema mkutano
kuhusu jumbe za Iran na Marekani utafanyika Geneva kuanzia tarehe 9 hadi
10 Juni.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi ataongoza
ujumbe wa Iran katika mazungumzo hayo huku ujumbe wa Marekani ukiongozwa
na Wendy Sherman Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani. Araqchi
amesisitiza kuwa mkutano wake na Sherman utahusu kadhia ya nyuklia
pekee. Mkutano huo unakuja kabla ya duru nyingine ya mazungumzo kuhusu
mpango wa Iran wa nishati ya nyuklia ambayo yanatazamiwa kufanyika Juni
16-20 katika mji wa Vienna nchini Austria. Maafisa wa Iran pia
wanatazamiwa kukutana na wanadiplomasia wa Russia huko Roma, Italia kati
ya Juni 11 na 12. Aidha maafisa wa Iran wanatazamiwa pia kufanya
mazungumzo na wawakilishi wengine wa kundi la 5+1 ambalo linajumuisha
China, Russia, Ufaransa, Uingereza, Marekani na Ujerumani. Iran imekuwa
ikifanya mazungumzo na madola hayo kwa lengo la kuondoa hitilafu
zilizopo kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran wenye malengo ya amani.






No comments:
Post a Comment