Baraza kuu la Umoja wa Mataifa limeafiki kuanzishwa kwa tuzo ya Nelson
Mandela kutokana na msimamo wake katika kusaka haki na usawa kwa wote.
Tuzo hiyo inalenga kuendeleza kazi aliyoitetea Mandela ya usawa wa
binadamu na haki zao kwa kuwatia moyo wale wanaosimamia misingi hiyo
ambayo pia Umoja wa Mataifa unazingatia.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
Ban Ki-moon amesema hiyo ni hatua nyingine zaidi ya Umoja wa Mataifa
kusongesha mbele kile ambacho Hayati Mzee Mandela alikiamini.
Mwakilishi wa kudumu wa Afrika Kusini kwenye Umoja wa Mataifa Balozi
Kingsley Mamabolo ametoa shukrani zake kufuatia uamuzi huo. Ameongeza
kuwa kwa kuridhia azimio kuhusu tuzo ya Mandela, Umoja wa Mataifa
umedhihirisha shukrani zake kwa dhima ongozi ya Mandela kwenye harakati
za ukombozi wa Afrika na Umoja wa Afrika. Shujaa Nelson Mandela, Rais wa
zamani wa Afrika Kusini na ambaye aliongoza mapambano ya miaka mingi
dhidi ya ubaguzi wa rangi nchini Afrika Kusini, alifariki dunia Desemba
mwaka jana akiwa na umri wa miaka 95.Shujaa huyo wa Afrika anaendelea
kukumbukwa kwa jinsi alivyojitolea kwa ajili ya ukombozi wa watu wake na
ataendelea kuwa kigezo kizuri cha ukombozi na kupigania haki.







No comments:
Post a Comment