Kanisa Katoliki duniani linakabiliwa na mashinikizo makali kuhusu
udhalilishaji wa watoto wadogo baada ya mtafiti kugundua mafuvu na
mifupa ya watoto taribani 800 wakiwa wamezikwa katika kaburi la umati
nchini Ireland.
Serikali ya Ireland imetangaza kuwa inatafakari kufanya uchunguzi
rasmi baada ya utafiti mpya kubaini kupata rekodi za watoto 796
waliopoteza maisha na kuzikwa katika makaburi yasiyo na alama huko
magharibi mwa nchi.
Watoto hao walirundikwa katika kaburi la umati lililo karibu na
nyumba ya mayatima iliyokuwa ikisimamiwa na watawa wa kike katika eneo
la Tuam, Kaunti ya Galway. Mayatima hao walikuwa wale waliozaliwa nje ya
ndoa. Watoto hao ambao baadhi walikuwa na umri wa siku mbili walipoteza
maisha kati ya mwaka 1924 hadi 1961. Rekodi zinaonyesha kuwa walipoteza
maisha kutokana na lishe duni, magonjwa na maradhi, ulemavu na kuzaliwa
kabla ya wakati. Uchunguzi unaonyesha kuwa watoto hao walitupwa katika
eneo lilokuwa na dimbwi la maji machafu. Dimbwi hilo liligeuzwa kuwa
kaburi la umati. Mashirika ya kutetea haki za binaadamu yamelitupia
lawama Kanisa Katoliki na kusema lilihusika na mauaji hayo ya umati.
Kanisa Katoliki Ireland limedai kuwa halina habari kuwa eneo hilo
lilikuwa kaburi la umati. Katika miaka ya hivi karibuni Kanisa Katoliki
limekuwa likilaumiwa vikali kwa kuwadhalilisha kijinsia watoto walio
chini ya usimamizi wake.







No comments:
Post a Comment