Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Saturday, December 28, 2013

Kuitwa magaidi Ikhwanul Muslimin, mkakati mwengine wa ramani ya njia ya wanajeshi nchini Misri

Serikali ya Misri iliyowekwa madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi imeitangaza Ikhwanul Muslimin kuwa ni kundi la kigaidi, katika hatua ya utekelezaji ramani ya njia iliyoandaliwa tangu yalipofanyika mapinduzi hayo dhidi ya Muhammad Morsi, rais halali wa nchi hiyo. Mnamo siku ya Jumanne ya tarehe 24 mwezi huu, gari moja lililotegwa bomu liliripuka kwenye kituo cha polisi cha mji wa Mansoura kaskazini mwa mji mkuu wa Misri, Cairo na kusababisha vifo vya watu wasiopungua 15 na kuwajeruhi makumi ya wengine. Muda mfupi baada ya mripuko huo Sharif Shaufi, msemaji wa Waziri Mkuu wa Misri Hazim al Beblawi, aliitangaza Ikhwanul Muslimin kuwa ni kundi la kigaidi.
Akimnukuu Waziri Mkuu huyo wa Misri Shaufi alidai kwamba kundi la Ikhwan limeonyesha sura yake chafu ya kigaidi kwa kumwaga damu na kuvuruga usalama wa Misri.
Hakuna asiyejua kwamba katika kipindi chote cha miaka 85 tangu kuasisiwa kwake harakati ya Kiislamu ya Ikhwanul Muslimin haijawahi kuuweka ugaidi katika ajenda ya utekelezaji wa ratiba na mipango yake. Kwa muda wote huo wa zaidi ya miongo minane, kwa mara kadhaa Ikhwanul Muslimin imepigwa marufuku na tawala tofauti za Misri, lakini haijawahi hata mara moja kufanya vitendo vya kigaidi na vya uripuaji mabomu au hata utumiaji nguvu dhidi ya tawala hizo. Kwa maana hiyo basi, ikiwa mripuko wa siku ya Jumanne uliotokea Mansoura hautokuwa umepangwa na serikali yenyewe ya muda ya Misri kwa lengo la kuionyesha Ikhwan kuwa ni harakati inayofanya vitendo vya kikatili ili kuweza kuifuta, basi utakuwa umetumiwa na serikali hiyo kama kisingizio cha kutimizia ndoto ambayo imekuwa nayo muda wote huu.
Muhammad Morsi, rais halali wa Misri aliondolewa madarakani tarehe 3 Julai mwaka huu kupitia mapinduzi ya kijeshi. Na kuanzia wakati huo ikaanza kampeni ya kuchukua hatua dhidi ya viongozi na wanachama wa Ikhwanul Muslimin kwa kuwatia nguvuni na kuwaweka korokoroni. Katika kuendeleza mkakati huo ulioratibiwa dhidi ya Ikhwan, serikali ya muda ya Misri ilichukua hatua ya kuivunja harakati hiyo. Katika awamu hii muhimu ya tatu, serikali hiyo imekamilisha mkakati wa kuifuta kikamilifu Ikhwanul  Muslimin kwa kuitangaza kuwa ni kundi la kigaidi.

Itakumbukwa kuwa baada ya kung'olewa madarakani dikteta Hosni Mubarak, Ikhwanul Muslimin ilidhihirisha wazi kuwa ndio harakati muhimu zaidi na yenye kupendwa zaidi na wananchi wa Misri baada ya kujipatia ushindi wa kishindo katika chaguzi zote tatu za kidemokrasia zilizofanyika nchini humo. Ni wazi kwamba hatua iliyochukuliwa dhidi ya Ikhwan, lengo lake ni kuizuia harakati hiyo muhimu isiwe na nafasi yoyote katika mazingira ya wakati huu ndani ya jamii ya Misri ambapo nchi hiyo inajiandaa kwa kura ya maoni ya katiba pamoja na uchaguzi wa rais na bunge. Kura ya maoni ya katiba mpya ambayo imeandaliwa bila ya kuishirikisha Ikhwanul Muslimin imepangwa kufanyika tarehe 14 na 15 za mwezi ujao wa Januari. Serikali ya mpito imekusudia pia kuitisha chaguzi za urais na bunge baadaye mwakani, ambapo Waziri wa Ulinzi Abdulfatah el Sisi aliyeongoza mapinduzi ya kijeshi dhidi ya Morsi ameonyesha nia ya kugombea katika uchaguzi ujao wa rais. Majenerali wa jeshi na viongozi wa serikali ya mpito wametekeleza mpango wa ramani yao ya njia wa kuifuta Ikhwanul Muslimin ili kuweza kuamua juu ya mustakabali wa mfumo wa kisiasa wa Misri kwa urahisi zaidi na pasina kukabiliwa na upinzani wowote wa kutia wasiwasi. Na lengo ni kuhakikisha serikali ijayo ya Misri itakayofanya kazi kwa muongozo wa wanajeshi si serikali ya mapinduzi ya kijeshi bali ni serikali iliyopatikana kwa kura za wananchi hata kama ni kwa uchaguzi ambao matokeo yake yalikwisha pangwa tangu kabla. Ili kufanikisha mkakati huo, sambamba na kutangazwa Ikhwanul Muslimin kuwa ni kundi la kigaidi, karibu vyama 30 na harakati kadhaa za kisiasa zimeasisi muungano uitwao "Harakati ya Kitaifa" ya kuunga mkono ramani ya njia ya mustakabali wa Misri pamoja na kuliunga mkono jeshi na polisi ya nchi hiyo. Lakini nukta muhimu na ya kutaamali hapa ni kwamba serikali ya muda ya Misri ilikitumia kisingizio cha mripuko wa bomu uliotokea siku ya Jumanne kwenye kituo cha polisi mjini Mansoura kuitangaza Ikhwanul Muslimin kuwa ni kundi la kigaidi, ilhali harakati hiyo ilitoa tamko rasmi la kulaani shambulio hilo, na badala yake kundi linalojiita Ansaru Baitul Maqdis likatoa taarifa siku ya Jumatano na kutangaza rasmi kuwa ndilo lililohusika na shambulio hilo

No comments: