Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Friday, June 7, 2013

Kuvunjika mazungumzo nchini Bahrain

Vyama na harakati za upinzani nchini Bahrain vimetangaza kuwa utawala wa Aal Khalifa hauna nia ya kuona mazungumzo ya nchi hiyo yanakuwa na tija; na kwa sababu hiyo mazungumzo hayo yamegonga mwamba.  Huku vikibainisha kuwa utawala wa Aal Khalifa umevitumia vikao 20 vya mazungumzo yaliyofanyika huko nyuma kwa ajili ya kupoteza muda na wala haujajali na kuzingatia mitazamo na matakwa yao, vyama na harakati za upinzani nchini Bahrain vimeeleza bayana kuwa lengo la utawala wa Manama ni kukwamisha malengo ya mapinduzi, lakini wananchi wa Bahrain wataendelea kuandamana kwa amani dhidi ya utawala wa Aal Khalifa hadi watakapopata matilaba na matakwa yao. Jamil Kadhim, mwanaharakati wa kisiasa nchini Bahrain amesema utawala wa ukoo wa Aal Khalifa unaendelea kutia nguvuni watu, kuwafunga, kuwatesa, kuvamia nyumba na maeneo ya kidini, kuwabagua na kutoa uraia kwa wageni ili kuvuruga muundo wa idadi ya watu, na kwamba jinai hizo zinafanywa huku jamii ya kimataifa na nchi za Kiarabu zikibaki kuwa watazamaji tu.
Khalil al Marzuq, Naibu Katibu Mkuu wa harakati ya Kiislamu ya al Wifaq anayehusika na masuala ya kisiasa amesisitiza juu ya ulazima wa kuhitimishwa dhulma na uonevu nchini Bahrain. Al Marzuq amesema Bahrain haitokuwa tena mahala pa kuendeleza dhulma na ukiritimba, kwa sababu mwenendo wa ukiritimba hauna tija nyengine ghairi ya uharibifu na kwamba wananchi wa Bahrain wameshaainisha njia wanayotaka kuifuata. Jawad Firuz, mwanaharakati wa upinzani nchini Bahrain ameeleza kuwa utawala wa Aal Khalifa unavitumia vyombo vya mahakama kama silaha ya kuwakandamizia wapinzani. Firuz, ambaye ni mbunge wa zamani katika bunge la Bahrain ameiambia kanali ya televisheni ya BBC ya Kiarabu kuwa jumuiya za kutetea haki za binadamu zina mtazamo mmoja juu ya suala hili kwamba hukumu zote za mahakama za Bahrain zinatolewa kwa lengo la kuwashinikiza kisiasa wanamapinduzi wa nchi hiyo. Upinzani wa wanaharakati wa kisiasa kwa ukandamizaji unaofanywa na utawala wa Aal Khalifa nchini Bahrain dhidi ya matakwa halali ya wananchi unadhihirishwa katika hali ambayo watu saba wamejeruhiwa katika mashambulio yanayoendelea kufanywa na vikosi vya usalama vya utawala huo wa kifalme dhidi ya raia wa nchi hiyo. Kwa mujibu wa kanali ya televisheni ya al Alam raia hao wamejeruhiwa katika mashambulio yaliyofanywa na vikosi vya usalama vya utawala wa Aal Khalifa vikishirikiana na majeshi vamizi ya Saudi Arabia dhidi ya waandamanaji katika maeneo ya Karazkan, Sitra na al Qaryah. Aidha raia 21 wametiwa nguvuni katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. Tangu mwezi Februari mwaka 2011 hadi sasa Bahrain inashuhudia maandamano ya amani ya wananchi wanaopigania mageuzi; lakini hadi sasa mamia ya watu wameshauawa na kujeruhiwa kutokana na ukandamizaji wa vikosi vya utawala wa Aal Khalifa vikishirikiana na vile vya Aal Saudi. Kwa mujibu wa nyaraka na ushahidi wa mashirika ya kutetea haki za binadamu wapinzani kadhaa wa utawala wa Aal Khalifa wameuawa kutokana na mateso, na makumi miongoni mwao wamebaki na vilema. Aidha akina mama kadhaa waja wazito mimba zao zimeharibika kutokana na athari ya kuvuta gesi ya sumu waliyopuliziwa na vikosi vya utawala wa Aal Khalifa katika maandamano ya amani ya kuupinga utawala huo kandamizi

No comments: