Enzi hizo hatukua na Ukimwi.
Magonjwa ya
zinaa hayakuua mtu. Dalili yake ilikuwa kuwashwa na kujisikia vibaya
wakati wa kwenda haja ndogo tu, basi. Yakikuzidia unazunguka zunguka
mitaani unanunua dawa rangi mbili- kidonge cha “tetracylene”- aghali
ndiyo; lakini kinamaliza kabisa tatizo. Baadaye miaka ya themanini Ukimwi ukatangaza ufalme. Ukimwi haukuponywa kwa kidonge kama hicho. Na hata baada ya miaka thelathini, Ukimwi
ulipoanza kutibika katika nchi zilizoendelea, haikua kidonge kimoja,
bali ni vingi. Tena bei yake si ya porojo. Sijasikia mtu anayeweza
kuingia tu sehemu akanunua msururu wa vidonge vya kutibu Ukimwi. Tiba
hii ilihimili, lakini haijaondoa kirusi, abadan.
Kawaida kirusi cha Ukimwi huwa kinamshinda
mwanadamu kwa vile hushambulia mfumo mzima wa “kinga maradhi” mwilini.
Ingekuwa kirusi hiki hushambulia tu, ingetosha kuzuilika kama ambavyo
virusi vingine huzuilika, kule kubadilika badilika kwake ndiyo kiini
cha zogo. Ndiyo maana Waswahili tulivyo wabunifu tukaukatia ugonjwa
majina kama ‘ngoma’, ‘bomu’ ‘mdudu,’n a kadhalika.
Lakini watafiti hawajalala. Karibuni wametangaza
kuanza kuelewa namna Kirusi cha Ukimwi kinavyotekeleza ufisi wake.
Waganga hao Dk Barton Haynes na John Mascola walifanya majaribio kwa
mgonjwa wa Ukimwi kutoka Afrika na kuchora ramani (“mapping”) ya
mwenendo mzima. Hatimaye, tiba iko karibu ndivyo jarida la VR-Zone.Com
la Marekani lilivyotangaza kwa hamasa juma lililopita.
Hoja niliyoieleza hapa inaonyesha namna matangazo ya tiba za magonjwa mbalimbali zinazowasakama wanadamu yalivyo muhimu.
Mbali na Ukimwi yapo maradhi yenye virusi
vikali,yanayoendelea kutusakama wanadamu, mathalan- Malaria, Saratani na
Kifua Kikuu kilichoanzakurejea karibuni...
Tatizo haliko katika haya maradhi bali katika sugu, ambayo virusi vimejenga. Sikilizeni kisa kifupi.
Takriban miaka 15 iliyopita nilipohamia hapa
Uingereza niliwahi kwenda zahanati ndogo ya kitongoji ninachoishi shauri
ya mafua makali. Kawaida mafua ni ugonjwa katili sana jamii hizi za
nchi baridi , huja majira yanapobadilika mwezi Mei kutoka msimu wa
baridi kuingia joto na Novemba ambapo joto kuisha na kipupwe kuanza.
Kufika kwa mganga akanipima presha, moyo, pumzi naye akasema niko sawa
kabisa.
“Lakini daktari silali, usiku kucha napiga chafya.”
Akaniangalia kwa macho yenye mseto wa huruma nacheko.
“Sikiliza. Wewe mzima kabisa bwa’ mkubwa; moyo na
mwili wako viko shwari shauri unafanya mazoezi, unajiangalia; huvuti
sigara,unajali unachokula, afya yako kama ya kijana wa miaka 20 (nilikua
na miaka arobaini). Nenda zako tu nyumbani kapumzike. Usitoke toke;
kunywa maji kwa wingi, lala kwa muda mrefu. Utapona tu.”
Duu, nikamwona mganga yule ambaye aliwahi pia kufanya kazi Tanzania kama ana mipango mibaya nami.
“Naomba unipe dawa kali daktari. Siwezi nikakaa nyumbani na mafua, bila dawa yeyote. Unajua mafua yanaua hapa kwenu Ulaya?”
Akacheka.
“Nimeifanya kazi hii karibu miaka 30. Usipende
sana kunywa kunywa dawa. Nenda zako tu nyumbani kapumzike. Baada ya siku
tatu ukiona hali mbaya rudi tena nitakupa hiyo dawa kali unayoitaka.”
No comments:
Post a Comment