Social Icons

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

Monday, July 1, 2013

Kuanza kujiandikisha wagombea urais nchini Mali

Mahakama ya Katiba nchini Mali, imesema kuwa watu 36 ya wameshajiandikisha kwa ajili ya kushiriki kwenye kinyang’anyiro cha uchaguzi ujao wa rais nchini humo. Wanne kati ya watu hao waliojiandikisha kugombea katika uchaguzi huo, ni mawaziri wakuu wa zamani na mawaziri wawili wanawake ambao waliwahi kuwa wawakilishi katika bunge la taifa hilo la magharibi mwa Afrika. Hii ni katika hali ambayo, Tiébilé Dramé, waziri wa zamani wa mambo ya nje wa Mali ambaye aliongoza ujumbe wa serikali ya mpito ya Bamako katika mazungumzo ya kusaka amani na kundi la Tuareg linalopigania kujitenga eneo la Azawad la kaskazini mwa Mali, huko mjini Ouagadougou, Burkinafaso, ni miongoni mwa watu wenye nia ya kushiriki kwenye kinyang’anyiro hicho.
Mahakama ya Katiba ya Mali itatangaza majina ya watu waliotimia masharti ya kugombea tarehe 7 Julai mwaka huu sambamba na kuanza kampeni za uchaguzi huo. Kwa mujibu wa wa muda ulioainishwa na serikali ya mpito ya Bamako,  uchaguzi wa rais unatakiwa ufanyike tarehe 28 mwezi huu wa Julai huku duru ya pili ya uchaguzi huo ikiwa imepangwa kufanyika tarehe 18 Agosti mwaka huu ikiwa italazimu kufanya hivyo. Pamoja na hayo Mamadou Diyamontin, Mkuu wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi ya nchi hiyo amesema kuwa, kwa sasa ni vigumu kupatikana watu milioni nane waliotimiza masharti ya kupiga kura katika uchaguzi huo. Hii ni kwa sababu karibu raia laki tano wa nchi hiyo wamekuwa wakimbizi kutokana na vita vya ndani. Aidha Diyamontin ameitaja hali ya ukosefu wa amani na utulivu wa kisiasa nchini humo hususan katika mji wa Kidal wa kaskazini mashariki wa nchi hiyo ambao hadi leo bado unadhibitiwa na waasi wa Kituareg, kuwa ni sababu nyingine inayokwamisha kufanyika uchaguzi huo wa rais. Pamoja na kuwepo makubaliano ya usitishaji vita kati ya serikali ya mpito na makundi ya watu wenye silaha wa kabila hilo la Tuareg, lakini hadi sasa bado majeshi ya nchi hiyo, yameshindwa kuingia katika mji huo uliotajwa. Wakati huo huo, Harakati ya Taifa ya Ukombozi ya Azawad ya kabila la Tuareg mjini Kidal, imesisitiza kuwa, hakuna kizuizi chochote kitakachoweza kuzuia kufanyika uchaguzi huo mjini humo. Baadhi ya duru zinatabiri kuwa, kufanyika uchaguzi katika hali ya mivutano iliyopo hivi sasa nchini Mali, kutapelekea serikali itakayochukua madaraka kutoka kwa utawala wa sasa wa mpito, kukosa nguvu. Aidha wachambuzi wa mambo wanaamini kuwa, kuwepo ujumbe wa vikosi vya Umoja wa Mataifa vya kulinda amani nchini Mali kinachojulikana kwa jina la MINUSMA, kutasaidia kufanikisha uchaguzi wa terehe 28 mwezi huu. Askari wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa wapatao 12600 ambao wengi wao wanatoka nchi za Afrika, wanaanza operesheni yao hiyo hii leo Jumatatu ya Julai Mosi. Imepangwa kuwa, vikosi hivyo vichukue jukumu la kulinda usalama na amani huko kaskazini mwa Mali kutoka kwa askari wa Ufaransa. Hivi sasa kuna askari 3,000 wa Ufaransa katika eneo hilo na inasemekana kuwa idadi hiyo itapungua hadi askari 1,000 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu wa 2013.

No comments: