Miongoni mwa changamoto zinazowakabili viongozi wa Saudi Arabia katika
miaka ya hivi karibuni ni kukiukwa haki za wanawake. Kuhusiana na suala
hilo, jambo ambalo limekuwa likiakisiwa zaidi na duru za habari katika
siku za hivi karibuni ni kufichuliwa habari ya kuteswa wanawake katika
jela za nchi hiyo. Wapinzani wa serikali ya Riyadh wamefichua kwamba,
maafisa wa jela ya al Swafraa nchini Saudia wanawatesa wanawake
wanaoshikiliwa kwenye jela hiyo.
Taarifa iliyosambazwa na wapinzani hao
inaeleza kuwa, maafisa wa jela hiyo iliyoko katika mji wa al Barida,
waliwalazimisha wafungwa 7 wa kike wa jela hiyo kutia saini makaratasi
ambayo haikujulikana yameandikwa nini na kisha kuwatesa. Hii si mara ya
kwanza kufichuliwa suala la kuteswa na kunyanyaswa wafungwa katika jela
za Saudia hasa wanawake. Nchi hiyo ya Kiarabu inaongozwa kwa sheria
zisizokuwa wazi. Watawala wa nchi hiyo ambao wengi wao ni wana wa
Abdulaziz muasisi wa ukoo unaotawala wa Aali Saud, katika miaka ya hivi
karibuni wameendelea kuitawala nchi hiyo kiimla. Katika nchi hiyo, kila
sauti ya mpinzani huzimwa lakini pengine tunaweza kusema kuwa, wanawake
wa Saudia ndio wanodhulimiwa zaidi. Hii ni kwa sababu hawana haki yoyote
ya kiraia, na ni miongoni mwa masuala yanayopelekea watawala wa Riyadh
kukosolewe sana. Amma suala lisiloweza kupingika ni hili kuwa, tangu
kuanza harakati za kimapinduzi za wananchi wa Saudi Arabia, haki na
uhuru wa kirai ambazo kwa miaka mingi zimekuwa zikikandamizwa kikamilifu
na watawala wa Aali Saudi zimeanza kuzingatiwa na kuakisiwa zaidi.
Miaka miwili na nusu imepita tangu harakati hizo zianze na katika
kipindi chote hicho wanawake pia wamekuwa wakishirikiana bega kwa bega
na wanaume katika kudai haki zao walizoporwa. Lakini watawala wa Riyadh
badala ya kuzingatia matakwa hayo, wanakabiliana na wananchi kwa
ukandamizaji. Katika miezi kadhaa iliyopita kumeripotiwa kuongezeka
idadi ya wafungwa nchini humo hasa wanawake. Baadhi ya takwimu
zinaonyesha kuwa, kuna wafungwa zaidi ya 30,000 nchini Saudia ambao
mustakbali wa wengi wao haujulikani. Wafungwa hao wa kike na wa kiume
wanakabiliwa na hali ya kusikitisha kama vile kushikiliwa muda mrefu
bila kuhukumiwa na wakati huo huo kuteswa. Hali hiyo inathibitisha
ukiukwaji wa wazi wa haki za binadamu nchini humo. Pamoja na hayo lakini
hadi sasa hakuna taasisi yoyote ya kimataifa ya kutetea haki za
binadamu iliyochukua hatua ya kulaani na kukabiliana na hali hiyo. Kimya
cha taasisi hizo kimepelekea watawala wa Aali Saudi wazidi kukiuka haki
za binadamu, kuwakandamiza wananchi na kuendeleza siasa za kibabe
nchini humo. Hata hivyo jambo hilo halijawavunja moyo wananchi wa Saudia
na wanasisitiza kuendelea na harakati zao za kimapinduzi ili kuleta
mabadiliko ya kisiasa na kudai haki zao muhimu zikiwemo za uhuru,
demokrasia na kuondolewa ubaguzi katika jamii ya nchi hiyo.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)







No comments:
Post a Comment